Sheria Leo. Ulinzi wa Kisheria dhidi ya Ukatili kwenye Mahusiano

Utangulizi

Karibu sana ndugu msomaji wa makala za Sheria Leo ambapo umekuwa ukipata maarifa juu ya sheria mbali mbali na dhana kadhaa za kisheria kila siku. Tumejifunza kwa muda mrefu juu ya makosa mbali mbali na namna ya kisheria kosa linavyotokea kwa kitendo na dhamira. Katika makala iliyopita tulianza kuangalia juu ya Jinai ya Kipigo kwenye mahusiano. Leo tunaendelea na sehemu nyingine juu ya Ulinzi wa Kisheria dhidi ya Ukatili kwenye Mahusiano.

Ulinzi wa Kisheria dhidi ya Ukatili kwenye Mahusiano

Ni jambo la kufahamu wa watu wote walio kwenye mahusiano iwe ya kindoa au mahusiano mengine, kwamba hakuna mtu anayemmiliki mwenzi wake. Kila mmoja ana haki ya kulindwa na Katiba na Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Katiba ya JMT inaeleza wazi wazi kuwa kila mwananchi anayo haki ya kuishi. Ibara ya 14 ya Katiba ya JMT inasema

kila mtu anayo haki ya kuishi na kupata hifadhi ya maisha yake kwa jamii kwa mujibu wa sheria’.

Maisha ni zawadi ambayo kila mwanadamu amepewa na Mungu, hivyo mifumo ya tawala za duniani kwa mujibu wa Katiba na sheria inawajibika kulinda na kutunza maisha ya kila mmoja wetu.

Kumekuwa na dhana ya kijamii kuwa mume anammiliki mwanamke kwa sababu tu ya utamaduni kuwa waume ndio wanaoa na kulipa mahari. Dhana hii imeleta madhara makubwa hasa kwa makundi ya wanawake katika kujikuta wananyanyasika na kudhalilika katika mahusiano. Maneno makali, vipigo na matishio ya mara kwa mara vimehusishwa sana na wanaume dhidi ya wanawake.

Mahusiano ya mume na mke au mapenzi kati ya mtu mume na mke, hayawezi kumpa mmoja wapo au wote haki ya kummiliki mwengine. Kila mmoja analindwa na sheria.

 

Mambo ya Msingi kuzingatia kwenye mahusiano ili kuepusha jinai ya kipigo;

  • Kufahamu msingi wa ulinzi wa Kikatiba na Kisheria kwa watu wote ikiwa ni pamoja na wanandoa au walio kwenye mahusiano
  • Walio kwenye mahusiano kutoona aibu au fedheha kutoa taarifa kwa watu au serikali au ustawi wa jamii juu ya vitendo vinavyoashiria ukatili dhidi ya utu wao

 

  • Jamii kutokunyamaza au kutokupuuzia matendo au viashiria vya unyanyasaji na ukatili katika mahusiano.

Endelea kufuatilia makala zinazokuja ili kujifunza hatua zinazopaswa kuchukua ili kupunguza tatizo hili la vipigo katika mahusiano.

 

Kumbuka kutokujua sheria si utetezi iwapo utatenda kosa lolote tafuta maarifa sahihi ya kisheria yakusaidie kufanya maamuzi sahihi kila siku.

Muhimu

Ikiwa una maswali au kuna eneo la kisheria ungependa kupata ufafanuzi basi nafasi ni yako na ndio msingi wa mtandao huu wa Uliza Sheria. Wasiliana nami na kuuliza maswali mbalimbali ili tuyachambue kwenye makala zijazo kwa njia ya e mail ulizasheria@gmail.com namba ya simu watsup 0713 888 040 na kwa sms .

Nakutakia siku njema.

Wako

Isaack Zake, Wakili