Fahamu Mambo ya Msingi kuhusu Kitendo cha Kijinai ‘Actus reus’

Utangulizi

Karibu sana ndugu msomaji wa makala zetu ambapo umekuwa ukipata maarifa juu ya sheria mbali mbali na dhana kadhaa za kisheria kila siku. Katika makala iliyopita kwenye tuliangalia juu ya kitendo cha kijinai na dhamira ya kijinai. Leo tunakwenda kuangalia tena kwa undani juu ya mambo ya msingi ya kuzingatia kuhusu Kitendo cha Kijinai.

Kitendo cha Kijinai

Kwa kuangalia makala zilizopita tulizungumzia juu ya viashiria vya kosa la jinai kuhusisha ‘kitendo cha kijinai’ na ‘dhamira ya kijinai’ yaani ‘actus reus’ na ‘mens rea’. Tumeona kwa mifano juu ya kitendo cha kijinai na namna ambayo kinafanya kazi.

Kitendo cha kijinai au ‘actus reus’ kinaweza kutafsiriwa kama tendo au kitendo ambacho sheria imekataza mtu kufanya. Tendo kinyume cha sheria.

Kwa mujibu wa sheria suala la kitendo cha kijinai linahusisha dhana kuu mbili yaani ‘kutenda kitendo kilichokatazwa na sheria’ au ‘kuacha kutenda kile ambacho unawajibika kutenda’. Kwa tafsiri ya kiingereza ina maana      ‘actus reus means an act or omission punishable by law’

Dhana hii tunaiona pia katika sheria ya Kanuni ya Adhabu Sura ya 16, Kifungu cha 5 kinachosema

Kosa ni kitendo, jaribio au kuacha kutenda kunakoadhibiwa na sheria

‘Offence is an act, attempt or omission punishable by law’

Mambo ya Msingi kuhusu Kitendo cha Kijinai

Katika kutafsiri kitendo cha kijinai vyombo vinavyohusika ikiwepo Polisi, Ofisi ya Mashitaka na Mahakama ni lazima kuzingatia mambo haya ya msingi kabla ya mtuhumiwa kutiwa hatiani kutokana na kitendo alichokifanya endapo kimekidhi vigezo vya kuhesabika kama kitendo cha kijinai au la.

  1. Kitendo cha Kijinai kwa maana ya Kitendo kinyume cha sheria ‘an act as actus reus

Katika kupata tafsiri halisi ya kisheria na kudhibitisha juu ya kosa la kijinai ni muhimu mahakama kujiridhisha kuwa mtuhumiwa alitenda kitendo cha kijinai. Kitendo hiki ni lazima kiwe kimekatazwa na sheria au kinyume cha sheria. Lazima uwepo ushahidi wa kutosha kuwa ni mtuhumiwa na si mtu mwengine alitenda tendo hilo.

Mfano;

Kifungu cha 130 cha Kanuni ya Adhabu Sura ya 16 kinatoa marufuku ya Kitendo cha Kubaka. Hivyo ili kosa hili lidhibitike ni lazima mtuhumiwa awe ametenda kitendo hicho kinyume na sheria. Kwa tafsiri ya sheria ni lazima mbakaji awe mwanaume.

  1. Kitendo cha Kijinai kwa maana ya Kuacha kutenda kwa mujibu wa sheria ‘ommission as actus reus’

Hapa mahakama inajikita katika kuangalia ni wajibu gani ambao mtuhumiwa alipewa kisheria kisha ni kwa jinsi gani hakutekeleza wajibu huo. Tunafahamu kuwa haki huambatana na wajibu na ili kupata haki lazima uhakikishe umetimiza wajibu.

Mfano;

Kifungu 167 cha Kanuni ya Adhabu Sura ya 16 kinaeleza juu ya ‘mtu mwenye wajibu wa kutoa matunzo kwa watoto ikiwa ni chakula, malazi, mavazi na huduma za kiafya, akiacha kutenda au kutekeleza wajibu huo anakuwa ametenda kosa la kijinai.

  1. Kitendo cha Kijinai na Hali ‘actus reus with circumstances’

Yapo makosa ya kijinai ambayo sheria inachukulia yamefanyika kutokana na hali ya mazingira. Mtuhumiwa anaweza asionekane amefanya kitendo fulani au ameacha kutenda kitendo bali mazingira aliyokutwa nayo yanaweza kuashiria kosa la kijinai.

Mfano

Katika sheria zinazohusiana na Usalama Barabarani, sheria inamtaka dereva awe katika hali nzuri ya uendeshaji wa chombo yaani asiwe katika hali ya kilevi, endapo itabainika kuwa anaendesha huku akiwa na kilevi basi atakuwa ametenda kosa la jinai. Hapa hatuoni dereva akitenda kosa la kunywa kilevi lakini anakutwa kuwa hawezi kuendesha au kukidhibiti chombo kutokana na matumizi ya kilevi aliyoyafanya hapo awali.

  1. Kitendo cha Kijinai na Kusababisha madhara ‘actus reus with causation’

Ni muhimu sana mahakama ikapata uchunguzi wa kutosha kuhusiana na kosa na endapo ni kitendo cha mtuhumiwa husika ndicho kilicholeta madhara kwa mwathiriwa. Kuna wakati unaweza kujitokeza kwa mtuhumiwa kutenda kitendo kinyume cha sheria lakini kisilete madhara kwa mwathiriwa na hivyo kukosekana kwa hatia. Hivyo ni lazima idhibitike kuwa ni kitendo cha mtuhumiwa ndicho kilicholeta madhara kwa mwathiriwa.

Mfano

A anakusudia kumuua B na anamwekea sumu kwenye chakula. B kabla ya kula chakula alichowekewa anapata mshtuko wa moyo na kufariki. A pamoja na kwamba alikusudia kumuua B kitendo alichofanya hakikusababisha kifo cha B hivyo hawezi kuhesabiwa hatia ya kumuua B.

Ndio maana ni muhimu sana linapotokea tukio la kifo lazima wachunguzi wafahamu sababu husika ya kifo.

Hitimisho

Leo tumejifunza mambo ya msingi kuhusu kitendo cha kijinai yaani ‘actus reus’ ambao vyombo vya uchunguzi, mashitaka na mahakama lazima vijiridhishe kuwa mtuhumiwa ndiye muhusika wa kufanya kitendo cha kijinai pasipo shaka. Wapo watu wengi wameingia katika hatia pasipo kujua au kukosa namna ya kujitetea au utetezi unaopaswa na kujikuta wanahukumiwa. Pia ni muhimu kwa jamii kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi kuadhibu watu pasipo kuwa na utaalam wa kujua endapo kitendo wanachodhani ni cha kijinai ikiwa kwa hakika kimetendwa na mtuhumiwa husika au la.

Endelea kufuatilia makala ijayo ili kujifunza zaidi juu ya kiashiria kingine cha kosa la kijinai.

Kumbuka kutokujua sheria si utetezi iwapo utatenda kosa lolote tafuta maarifa sahihi ya kisheria yakusaidie kufanya maamuzi sahihi kila siku.

Muhimu

Ikiwa una maswali au kuna eneo la kisheria ungependa kupata ufafanuzi basi nafasi ni yako na ndio msingi wa mtandao huu wa Uliza Sheria. Wasiliana nami na kuuliza maswali mbalimbali ili tuyachambue kwenye makala zijazo kwa njia ya e mail zakejr@gmail.com namba ya simu watsup 0713 888 040 na kwa sms .

Nakutakia siku njema.

Wako

Isaack Zake, Wakili

1 reply

Comments are closed.