Aina ya Dhamira za Kijinai ‘Kinds of Mens rea’

Utangulizi

Karibu sana ndugu msomaji wa makala zetu ambapo umekuwa ukipata maarifa juu ya sheria mbali mbali na dhana kadhaa za kisheria kila siku. Katika makala iliyopita kwenye tuliangalia juu ya Mambo ya Msingi ya Kitendo cha Kijinai. Leo tunakwenda kuangalia tena kwa undani juu ya Aina ya Dhamira za Kijinai ‘Kinds of Mens rea’

Dhamira ya Kijinai

Tumeona katika makala zilizotangulia juu ya umuhimu wa kiashiria cha kosa ni muhimu kwa dhamira ya kijinai kudhibitika mbali na kitendo cha kijinai peke yake. Dhamira ya kijinai inazungumzia hali ya kifikra ya mtuhumiwa wakati anatenda kosa husika.

Tuliona msisitizo huu katika maneno haya ya Kiingereza

‘the act itself does not constitute guilt unless done with a guilty intent’

Maneno haya yakimaanisha kuwa kitendo pekee cha kijinai hakiwezi kuonesha hatia mpaka kiwe kimeambatana na dhamira ya kijinai.

Aina ya Dhamira za Kijinai

Katika somo la leo tunaendelea kujifunza zaidi juu ya msingi wa mahakama kuchunguza kuhusu aina za dhamira za kijinai katika kufikia maamuzi juu ya kesi mbele yake. Katika mfumo wa kuchambua makosa na namna dhamiri ya kijinai ilivyohusika na kiwango cha adhabu atakachopata mtuhumiwa dhamira hizi zimegawanywa katika makundi yafuatayo;

  1. Dhamira ya Makusudi ya Kijinai ‘Intentional mens rea’

Aina ya dhamira hii ya makusudi ni ile ambayo inaonesha kuwa mtuhumiwa alikusudia kutenda kosa alilotenda kwa utashi wake huku akijua kitendo anachofanya ni cha kihalifu na kina madhara kwa mwathiriwa. Katika kupima endapo dhamira ilikuwa kusudi ni lazima kuona kuwa

  • Mtuhumiwa anajua matokeo ya kitendo anachofanya; hii ina maana mtuhumiwa anajua madhara ya kile kitendo anachokusudia kufanya. Mfano mtu anaiba fedha anajua matokeo yake ni hasara kwa mwathiriwa wa kuibiwa.
  • Mtuhumiwa anakusudia matokeo hayo ya kitendo chake yatokee; hapa ina maana mtuhumiwa kwa kujua kwake matokeo ya kitendo chake anakusudia kuyaona au kuyafikia matokeo hayo. Mfano mtuhumiwa anaiba kwa kusudi la kumnyang’ang’anya mwathiriwa haki ya mali yake. Katika kuainisha makosa ya makusudi ni muhimu sheria inayotamka kosa husika ioneshe dhamira ya kosa la makusudi. Mfano ‘kwa kukusudia’ ‘kwa utashi’ n.k

Katika shauri la Brazila vs Jamhuri la 1968, mtuhumiwa alikuwa karani wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba na alikuwa mwangalizi wa wafungwa waliokuwa katika Mahakama ya Mwanzo kwa mashauri yao. Aliwatoa wafungwa wawili kwenye chumba cha mahabusu na kuwaamuru kufua nguo zao naye akaenda kutembea wafungwa wakatoroka. Mtuhumiwa alishitakiwa kwa kosa la kusaidia wafungwa kutoroka kinyume cha Kifungu 117 (1) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu akahukumiwa kifungo. Wakati wa rufaa Jaji wa Mahakama kuu Mustafa aliangalia sheria na kifungu alichoshitakiwa nacho na kuona kuwa kilihitaji dhamira ya makusudi kudhibitishwa hivyo akabatilisha hukumu na kuhukumu kuwa mtuhumiwa alikuwa mzembe wa hali ya juu.

  1. Dhamira ya Uzembe uliokithiri ya Kijinai ‘ Recklessness mens rea’

Hapa dhamira ya uzembe uliokithiri hutokea katika mazingira ambayo mtuhumiwa anajua kuwa kutokana na kitendo chake kuna uwezekano mkubwa wa madhara kutokea lakini hayuko tayari kuyataka matokeo ya kitendo chake anachofanya. Kiwango cha uzembe huu uliokithiri katika kudhibitisha shitaka adhabu yake inakuwa tofauti na ile ya dhamira ya makusudi.

Mfano.

Dereva wa gari anaendesha gari pasipo kufuata sheria za barabarani haendi kwa mwendo unaopaswa kisheria na anadharau taa za barabarani matokeo yake kamgonga mtembea kwa miguu na kufa papo hapo. Dereva huyu pamoja na kwamba ameua lakini hatoshitakiwa kwa kosa la kuua kwa makusudi bali uendeshaji wa uzembe uliokirithi na kusababisha kifo cha mtembea kwa miguu.

  1. Dhamira ya Uzembe ya Kijinai ‘Negligence mens rea’

Hii ni aina nyingine ya dhamira ya kijinai ya uzembe ambapo mtuhumiwa haoni athari ya moja kwa moja ya matokeo ya kitendo anachofanya au anachoacha kufanya lakini kwa mtu wa kawaida alipaswa kufahamu kuwa kitendo chake kina madhara.

Katika shauri la Jamhuri vs Chape Kalangari la 1973 mtuhumiwa alishindwa kumuhudumia mtoto ambaye alikuwa anamtunza ambaye alikuwa anasumbuliwa na mafua makali. Kutokana na kutopata matunzo na usaidizi wa matibabu mtoto akafariki. Mahakama ilimpata mtuhumiwa na kosa la kuua kwa kutokukusudia sawa na Kifungu cha 203 cha Kanuni ya Adhabu. Mahakama ilisema kuwa ili mtu akutwe na hatia ya mauaji pasipo kukusudia kwenye mazingira haya ni lazima awe na wajibu wa kisheria wa kutimiza.

Hitimisho

Leo tumejifunza juu ya aina za dhamira ya kijinai ambazo ni makusudi, uzembe uliokithiri na uzembe. Mahakama ni lazima ijiridhishe juu ya aina ya dhamira inayohitajika katika kila kosa kabla ya kumhukumu mtu kuwa na hatia. Hivyo unapokuwa umetenda kosa au kuna mtu ametenda kosa ni muhimu kupata ushauri wa wanasheria kujua ni kwa mazingira gani kosa hilo limetendeka na endapo adhabu yake itakuwa ya namna gani kuweza kuandaa utetezi wako vizuri au utetezi wa mtuhumiwa vizuri.

Endelea kufuatilia makala ijayo ili kujifunza zaidi juu ya kiashiria kingine cha kosa la kijinai.

Kumbuka kutokujua sheria si utetezi iwapo utatenda kosa lolote tafuta maarifa sahihi ya kisheria yakusaidie kufanya maamuzi sahihi kila siku.

Muhimu

Ikiwa una maswali au kuna eneo la kisheria ungependa kupata ufafanuzi basi nafasi ni yako na ndio msingi wa mtandao huu wa Uliza Sheria. Wasiliana nami na kuuliza maswali mbalimbali ili tuyachambue kwenye makala zijazo kwa njia ya e mail zakejr@gmail.com namba ya simu watsup 0713 888 040 na kwa sms .

Nakutakia siku njema.

Wako

Isaack Zake, Wakili