Sheria Leo. Jinai ya Kipigo kwenye Mahusiano

Utangulizi

Karibu sana ndugu msomaji wa makala za Sheria Leo ambapo umekuwa ukipata maarifa juu ya sheria mbali mbali na dhana kadhaa za kisheria kila siku. Tumejifunza kwa muda mrefu juu ya makosa mbali mbali na namna ya kisheria kosa linavyotokea kwa kitendo na dhamira. Leo tunaenda kuangalia juu ya Jinai ya Kipigo kwenye mahusiano.

Makosa ya Kijinai

Katika makala za mwanzo kabisa tulijifunza juu ya makundi ya sheria na mojawapo ni kundi la Sheria za Jinai. Makosa ya kijinai ni aina ya makosa ambayo mtu akifanya anashtakiwa na Jamhuri/Serikali na matokeo yake endapo atapatikana na hatia basi anaweza kupata adhabu ya kifungo au faini au adhabu nyingine yoyote kwa mujibu wa sheria.

Kwa siku za karibu kumeongezeka makosa mengi au kumekuwa na wimbi kubwa la utendaji wa makosa ya kijinai hasa yanayohusiana na mahusiano baina ya mume na mke au wapenzi yaani watu walio kwenye uhusiano.

Tumesikia utendaji wa makosa haya kwenye vyombo vingi vya habari juu ya mume kumpiga mke hata kusababisha ulemavu au kupelekea mauti. Tumesikia mauaji ya kutisha ya kifamilia kwa sababu zinazoelezwa kuwa ni ‘wivu wa mapenzi’ n.k

Kama jamii na wadau tunaoishi ndani ya jamii hii tunapaswa kujiuliza tumefikaje hapa na katika hali hii na ipi njia nzuri ya kuweza kupunguza au kuepusha madhila haya ndani ya jamii zetu ambayo yameacha simanzi kubwa sana.

Msingi wa Mahusiano

Sheria ya Ndoa ya 1971 inatambua kuwa watu wanaweza kuwa kwenye mahusiano ya kindoa. Kwamba uhusiano huu ni wa hiyari baina ya mwanamke na mwanaume ambao wamefikia umri mwafaka wa kuamua kuishi pamoja.

Sheria ya ndoa inatambua kutokana na jamii yetu zipo ndoa ambazo zinafungwa kiserikali yaani bomani, zipo zinazofungwa kwenye nyumba za ibada yaani makanisani na misikitini na zile ambazo zinafungwa kimila. Zote hizi ni ndoa na halali kwa jamii kuzitambua.

Hatahivyo, ipo dhana ya ndoa ambayo inatambuliwa na sheria endapo mtu mume ataishi na mtu mke kwa kipindi kisichopungua maika 2 na kuonekana mbele ya jamii kama mke na mume watachukuliwa katika hali hiyo mpaka pale itakapodhibitika vinginevyo.

Msingi huu wote unaooneshwa kwenye sheria yetu ya ndoa ya 1971 inadhihirisha kuwa jamii yetu kwa ustaarabu wake na kuheshimu utashi wa watu wawili kuwa pamoja umeweka mazingira yote yanayowezekana ili watu hawa waishi kwa amani kwa hiyari yao wenyewe.

Katazo la ukatili katika mahusiano

Sheria ya ndoa ya 1971 inatoa onyo kwa pande zote kuwa ukatili katika ndoa unaweza kusababisha ndoa kuvunjika. Vipigo, manyanyaso na mambo mengine ya kikatili yanaweza kusababisha ndoa kuvunjwa na mahakama.

Hatahivyo, kama jamii tumekuwa tukishuhudia ukatili mkubwa ndani ya mahusiano ya kindoa na hata sasa ukatili au vipigo hivyo vimepitiliza hata kwenye mahusiano ya ‘boy friend’ na ‘girl friend’ kitu ambacho si sawa. Tunachokuja kushuhudia mwisho wa siku ni watu kuumizwa, kupata ulemavu na hata kupoteza maisha.

Kama jamii tunao wajibu mkubwa wa kuona tatizo hili na kuchukua hatua madhubuti ya namna bora ya kisheria kukabiliana nalo.

Endelea kufuatilia makala zinazokuja ili kujifunza hatua zinazopaswa kuchukua ili kupunguza tatizo hili la vipigo katika mahusiano.

 

Kumbuka kutokujua sheria si utetezi iwapo utatenda kosa lolote tafuta maarifa sahihi ya kisheria yakusaidie kufanya maamuzi sahihi kila siku.

Muhimu

Ikiwa una maswali au kuna eneo la kisheria ungependa kupata ufafanuzi basi nafasi ni yako na ndio msingi wa mtandao huu wa Uliza Sheria. Wasiliana nami na kuuliza maswali mbalimbali ili tuyachambue kwenye makala zijazo kwa njia ya e mail zakejr@gmail.com namba ya simu watsup 0713 888 040 na kwa sms .

Nakutakia siku njema.

Wako

Isaack Zake, Wakili