Sheria Leo. Je, Unamshtaki Nani?

Utangulizi

Karibu sana ndugu msomaji na mfuatiliaji wa ukurasa huu wa Sheria Leo kwenye mtandao wako wa Uliza Sheria. Kama kawaida yetu lengo la kukuletea makala hizi fupi ni kukusaidia kuishi kwa mujibu wa sheria kila siku. Leo tunajiuliza swali muhimu sana katika masuala ya mashauri ya mahakamani Je, unamshtaki nani?. Karibu tujifunze.

Mfumo wa Mashauri

Katika suala la kudai haki mahali au kwa mtu fulani, mara nyingi mchakato unaohusisha kwenda katika vyombo vya maamuzi haukwepeki yaani mahakama. Mfumo wetu wa kudai na kutoa haki unasimamiwa na Mhimili wa Dola unaoitwa Mahakama. Kazi kubwa ya mahakama ni kusikiliza mashauri mbali mbali na kutoa tafsiri sahihi ya sheria kama zilivyotungwa na Bunge.

Pande mbili zinazotafuta au kudai haki mbele ya mahakama zinatarajiwa kuleta hoja na ushahidi wa kusaidia ushindi au kupata haki wanayostahili. Ni wajibu wa kila upande kujiandaa na kujipanga endapo unashitaki au kushtakiwa, mahakama haina upande wowote bali kazi yake ni kuangalia ni upande gani una haki kisheria.

Je, unamshtaki nani?

Nieleze kisa kimoja ambapo mwananchi mmoja alifanya kesi kwa takribani miaka 3 na kushinda kesi husika dhidi ya mdaiwa wake. Hata hivyo mara baada ya kupata ushindi wa kesi hiyo, utekelezaji wa amri ya mahakama ulishindikana kwa sababu majina halisi ya mdaiwa na yale yaliyowasilishwa kwenye hati ya madai yalitofautiana.

Hiki ni kisa kimoja tu, miongoni mwa visa hivi vinavyotokea mahakamani kila siku.

Mojawapo ya vigezo vikubwa sana katika uendeshaji wa mashauri mahakamani ni kuhakikisha unamshitaki mtu sahihi na si vinginevyo. Watu wengi, hata wajuzi wa sheria huwa wanapata changamoto hii ya kushindwa kumshitaki mtu au taasisi sahihi. Umakini mkubwa unahitajika pale ambapo umefikia hatua ya kufungua shauri mahakamani kwa lengo la kudai haki yako.

Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Madai inamtaka mlalamikaji anayefungua shauri kuhakikisha anafungua shauri dhidi ya mdaiwa kwa majina yake halali ya kisheria.

Kesi nyingi na madai mengi ya wadai yameshindwa mahakamani kwa sababu mdai hakufanya kazi yake ya msingi kujua majina halisi ya mdaiwa. Ni muhimu sana ukiwa mdai kuhakikisha ya kwamba unamdai au kumshtaki mtu sahihi au taasisi sahihi kwa majina sahihi ili uweze kupata haki yako.

Msisitizo huu tunaweza kuuona katika shauri la rufaa lililofanyika mahakama ya rufaa baina ya CHRISTINA MRIMI na COCA COLA KWANZA BOTTLES LTD, rufaa  Na.112 of 2008, ambapo Mahakama ya Rufaa ilieleza yafuatayo, ninukuu kwa lugha ya kiingereza

‘Companies, like human beings, have to have names. They are known and differentiated by their registered names. In the instant case, it is apparent that the names ‘Coca Cola Kwanza Bottles’ Coca Cola Kwanza Ltd’ or ‘Coca Cola Bottlers Ltd’ have been used inter changeably. Although the Appellant wants this Court to hold that they mean one and the same Company, strictly, this view cannot be accepted without same risk of inexactitude.’

Tafsiri isiyo rasmi inasema

Kampuni ni kama wanadamu, zina majina na zinajulikana na kutofautishwa kwa majina katika kesi ya sasa majina kama Coca Cola Kwanza Bottles’ Coca Cola Kwanza Ltd’ au ‘Coca Cola Bottlers Ltd’ yamekuwa yakitumiwa mara kwa mara. Ingawa mrufani anataka mahakama hii iseme kuwa majina haya yote yanamaanisha ni kampuni moja, mtazamo huu hauwezi kukubalika bila kuleta athari kubwa’

Kisheria kumshitaki mtu anayeitwa JOHN JOSEPH JOHN na JOSEPH JOHN JOSEPH ni watu wawili tofauti.

Hitimisho

Ni muhimu sana kwako mdai mara zote kuhakikisha kuwa unamshitaki mdaiwa kwa majina yake sahihi. Tumeona mifano ya watu wengi wakikosa haki au haki yao ikichelewa kutokana na kukosea au kutokufanya utafiti wa kutosha juu ya yule anayetakiwa kushtakiwa.

Kumbuka ‘kutokujua sheria si utetezi iwapo utatenda kosa lolote’ tafuta maarifa sahihi ya kisheria yakusaidie kufanya maamuzi sahihi kila siku.

‘Usikwame kwenye tatizo lolote la kisheria wakati unayo nafasi ya kuuliza, uliza sheria uoneshwe njia’

Nakutakia siku njema sana ndugu yangu.

Mwandishi Isaack Zake ni wakili wa kujitegemea anayefanya katika ofisi za Uwakili Zake Advocates zilizopo Dar es Salaam, Mtaa wa Bibi Titi Mohamed. Isaack Zake anatoa elimu ya kisheria, ushauri wa kisheria katika maeneo mbalimbali kama Sheria za Kazi, Mirathi, Ndoa, Mikataba na Biashara. Kwa ushauri usisite kuwasiliana naye kwa 0713 888 040 na email zakejr@gmail.com

1 reply
  1. MAHAMOUD M Chande
    MAHAMOUD M Chande says:

    Hongera saan kaka Kwa kazi hii…nimekusoma nimeelewa. Kiukweli wananchi wengi tunashindwa kupata haki zetu Kwa kukwepa kuwapaleka watuhumiwa kwenye vyomb husika kwakuwa hatujui njia ya kuanzia…Na hata ukitafut utaratibu utapiti vikwazo vingi vinavyokuvuja moyo.

Comments are closed.